Wednesday 11 November 2015

HEKIMA YA KUJIBU MASWALI

Na Mchungaji Gakobwe,

Leo, tunajifunza Biblia kutoka katika MATHAYO 21:23-46.  Ingawa somo letu ni “HEKIMA YA KUJIBU MASWALI”, hata hivyo, kuna mengi zaidi ya kujifunza katika mistari hii.  Katika mistari hii, tunapata mambo manne tofauti, ya kujifunza:-
(1)      HEKIMA YA KUJIBU MASWALI (MST. 23-27)
Yesu Kristo, alikuwa na hekima ya kipekee katika kujibu maswali aliyokuwa anaulizwa kiasi ya kwamba watu hawakuthubutu kumwuliza maswali (MATHAYO 22:46).  Hatupaswi kujibu kila swali tunaloulizwa, kwa mfumo uleule.  Maswali mengine hayahitaji majibu yetu kabisa (YOHANA 19:8-9; MATHAYO 27:12-14), na majibu ya maswali mengine, ni kuwauliza maswali hao waliotuuliza (MATHAYO 21:23-27).  Kabla ya kujua hatua ya kuchukua tunapokabiliwa na swali, ni muhimu kwanza kuifahamu NIA ya swali lile tuliloulizwa, na pia aina ya swali lile.  Maswali tunayoulizwa, yako katika namna sita zifuatazo:-

1.     MASWALI YA MTEGO (MATHAYO 22:15-17) – Ni muhimu kujihadhari katika kujibu maswali ya jinsi hii, ili kujibu kwetu kusitufanye tunaswe katika mtego tuliowekewa na mtu anayeuliza swali.

2.     MASWALI YENYE NIA YA KUTUJARIBU (MATHAYO 19:3; LUKA 10:25) – Maswali haya huwa yana lengo la kutujaribu ufahamu wetu, kutujaribu kwamba tutajibu namna gani, ili anayeuliza swali, apate nafasi ya kutulaumu, kutushtaki au kupeleka taarifa mbaya mahali fulani.  Inahitajika tahadhari katika kujibu maswali haya.

3.     MASWALI YENYE NIA YA KULETA MADHARA (MATHAYO 2:3-8) – Kwa kutoa jibu kamili la maswali ya jinsi hii, tunaweza tukampa mtu yule aliyetuuliza, nafasi ya kufanya madhara aliyoyakusudia moyoni.  Mwizi anaweza kuuliza, Je, mtu huyu huwa anarudi jioni kutoka kazini kila siku?  Nikija asubuhi ni vigumu kumkuta?  Nyumbani kwake hakuna yeyote anayebaki?  Inahitajika tahadhari katika kujibu maswali ya namna hii.  Maswali ya kuleta shari, pia hatupaswi kuyajibu.

4.     MASWALI YENYE NIA YA KUJIDAI (LUKA 10:29) – watu wengine, siyo kwamba wanauliza kwa kutaka kuelimishwa, la, hasha.  Wao wanajidai kwamba ni wenye elimu kutupita na hivyo wanauliza maswali ili kutafuta kosa kwetu, halafu wao watuonyeshe kujua kwao.  Inatupasa kuwa na tahadhari.  Tusijibu maswali kwa nia ya kutafuta mashindano ya “Nani anajua zaidi”, tutafute zaidi kujibu maswali ya kumfanya mtu aache uovu.  Kujibu swali la maana ya vitasa, mihuri na baragumu za Ufunuo wa Yohana kutoka kwa mtu ambaye hajaookoka au ambaye hajaishi sawasawa na misingi ya Utakatifu, ni kupoteza muda wetu bure (2 TIMOTHEO 2:14, 16-18).

5.     MASWALI YA UPUMBAVU NA UPUUZI, YASIYO NA ELIMU (2 TIMOTHEO 2:23; TITO 3:9) – Maswali yoyote ya kuzua ugomvi au majadilianao ya kipuuzi tunapaswa kuwa mbali nayo.  Tunapokuwa tunawashuhudia watu habari ya wokovu, tuepuke maswali yao yanayohusiana na mafundisho ya ndani – Utatu wa Mungu, Uwana wa Mungu, Malipizo ya Ndoa, Mavazi ya mtu aliyeokoka, Ubatizo n.k.  Tuwaeleze tu njia ya kushinda dhambi na kukwepa maswali mengine.  Watafahamu hayo BAADA ya kuokoka.  Mtu haanzi darasa la saba, anaanzia darasa la kwanza.  Maswali ya upuuzi kama “Mungu alitokea wapi”, n.k., tuyakatae.  Kabla ya mtu kujua Mungu ametokea wapi, ajifahamu kwanza yeye ametokea wapi!

6.     MASWALI YENYE NIA YA KUJIFUNZA (MATHAYO 19:25-29; LUKA 20:27-37) – Maswali haya yana nia njema, hata hivyo, inatubidi kuangalia kwanza kiwango cha kiroho cha mtu.  Mtoto mdogo wa miaka mitano akiuliza  “watoto wanatoka wapi?”, huwezi kumjibu kwamba wanatokana na tendo la ndoa!  Kufanya hivyo ni kumpeleka mbali na maadili safi.  Vivyo hivyo, watoto wachanga kiroho, tuwajibu maswali ya kuwajenga tu katika uchanga wao.  Tuwape maziwa, na kamwe, tusiwape mifupa (WAEBRANIA 5:12-14; 1 PETRO 2:2).
JINSI YA KUPATA HEKIMA YA KUJIBU MASWALI – Inahitajika hekima ya Mungu katika kujibu Maswali.  Tukiipata hekima hii, tutafahamu upesi nia ya swali na kujua jinsi ya kulikabili swali hilo mara moja.  Hekima hii inapatikana kwa kuiomba kwa Mungu kwa imani kwamba atatupa, ili tumtumikie vema (YAKOBO 1:5-7).

No comments:

Post a Comment